Wataalamu wa sheria na mambo ya katiba serikalini walipotoa Hadidu za Rejea na kuikabidhi Tume ya Jaji Warioba kwa kupitia mkono wa Rais Kikwete, kuna wengine walidhani safari ya kisiasa kupata Katiba Bora waliyokuwa wanasafiri bila kufahamu walipo na wanakoenda, basi watakuwa wamefika.
Mwingereza anayejulikana kwa jina la kalamu kama Lewis Carroll alishawahi kusema, If you don’t know where you’re going, any road will get you there.
Well, kuna wanasiasa hawakufahamu kwa nini Hadidu za Rejea zilikuja na misingi kumi ambayo iliambatana na sheria ya mabadiliko ya Katiba 2013 iliyoacha milango ya kisheria wazi ambayo kwa sasa inatafsiliwa kwa namna yoyote bila hata kuvunja sheria. Wengine wanasema kazi ya Bunge la Katiba ni koboresha, huku wengine wakisema, kazi yake haina mipaka kisheria.
Majibu yake kwa sasa ndiyo haya yameanza kujitokeza kutoka kwa viongozi wakuu wandamizi wa serikali. Kama kuna viongozi wa siasa au vyama hawakufahamu kusuka au kunyoa lakini kwa sasa wako kwenye Bunge la Katiba, basi acha wanyolewe au wasukwe na serikali ya CCM ili wajitambue katika nafasi zao za kisiasa.
Waziri Mkuu ni mjumbe tu kwenye Bunge la Katiba pamoja na kwamba ni Mwenyekiti wa wabunge wa CCM lakini huwezi kuondoa msingi wa athari za matamko yake katika jamii. Kwa sasa yuko pale kutetea hoja na sera ya chama chake ambacho kina wanachama 'milioni tano'.
Hii ndiyo habari ya Mjini. Mnaotaka Serikali ya Tanganyika, mnakusudia Tanganyika ipi?. Tanganyika ya mkoloni au ya baada ya uhuru ya miaka mitatu!,
Mimi ninachotaka ni kuvunja Muungano au kama haiwezekani, basi serikali moja itanitosha kwa miaka 50 ijayo. Siitaki Tanganyika kwa sababu zijawahi kuiona. Sihitaji serikali mbili kwa sababu hazijajenga mazingira halisi ya serikali mbili. Serikali tatu ni kupoteza muda tu kwa sababu haziwezi kudumu. Serikali nne ni kuongeza gharama wakati shule hazina hata ubao wa kufundishia achilia mbali chaki na madawati.
Unapoona wingu linatanda, huna budi kutarajia mvua kunyesha lakini vile vile disappointment is all part and parcel of Homo sapiens.
Mizengo Pinda: Mnaitaka Tanganyika ipi?.
WAZIRI Mkuu Mizengo Pinda amekiri kuwa Bunge Maalumu la Katiba, limeanza na changamoto, huku akihoji wanaotaka Serikali ya Tanganyika, wanakusudia ipi ya mkoloni au ya baada ya uhuru ya miaka mitatu.
Mbali na hilo, amesisitiza yeye na chama chake cha Mapinduzi wanataka mfumo wa serikali mbili na si tatu kama Rasimu ya Katiba ilivyopendekeza.
Amekiri kuwa uchaguzi wa Mwenyekiti wa Bunge unaotarajiwa kufanyika wiki ijayo, utakuwa na misukosuko mingi, lakini utavuka salama.
Pinda aliyasema hayo jana wakati akifungua semina ya viongozi na watendaji wa Jumuiya ya Wazazi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), kwenye Makao Makuu ya chama hicho, White House mjini hapa.
Pinda ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, alisema zipo hoja nyingi za msingi katika mchakato huo wa kutunga Katiba, lakini kubwa na litakalochukua muda mwingi ni muundo wa Serikali. Hata hivyo, alisema wazi msimamo wake na ule wa CCM kuhusu pendekezo lao la kuwa na Serikali mbili, kinyume cha Rasimu ya Katiba inayopendekeza Serikali tatu.
“Hata ukiniamsha usingizini usiku wa manane, kwangu mimi bado Serikali mbili ni muundo mahsusi.
“Mwalimu Nyerere hata wakati ule alikaa na Tanganyika kwa kipindi kifupi, mwaka 1961 Tanganyika ikawa huru, 1962 tukawa Jamhuri, 1963 Zanzibar ikapata uhuru (baadaye alisema Uhuru wa bandia), mwaka 1964 ikazaliwa Tanzania.
“Tanganyika ya kikoloni ndiyo iliyokaa muda mrefu, hii nyingine ni kutoka mwaka 1961, 1962 na 1963. Ikazaliwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Leo hii miaka 50 tuko ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tunadai Tanganyika,” alihoji Pinda na kuongeza:
“Tanganyika ipi? Nikadai ile ya mkoloni? Kipi kimo katika Tanganyika ya miaka mitatu? Tanganyika wakati inazaliwa nilikuwa na miaka 13, Tanzania nilikuwa na miaka 16, naujua vizuri Muungano. Kuanzia pale sijui chochote kingine, kama ilivyo wengi wetu humu.
“Au wale waliozaliwa miaka 50 iliyopita, wanaijua vizuri zaidi Tanzania. Tanganyika ipi mnazungumzia? Maana haikuwapo zaidi ya ile ya kikoloni iliyokaa muda mrefu.”
Alisema njia bora ni kukaa chini na kuzungumzia matatizo ya muundo wa Serikali mbili na kuyaboresha kwa nia ya kusonga mbele kuliko kudai Serikali ya Tanganyika. Waziri Mkuu alisema si vyema kuanza sasa kujaribu muundo wa Shirikisho baada ya miaka 50 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, huku akitolea mfano wa Shirikisho la Afrika Mashariki (EAC).
“Pale kuna Shirikisho la Afrika Mashariki, lakini angalia mambo yanavyokwenda sasa wakubwa wakikutana. Utasikia wanazungumzia ardhi, mara pasipoti.
“Haiwezekani miaka 50 baada ya Muungano tuanze majaribio ya Shirikisho. Aah, wapi tunataka kwenda. Tanzania Bara na Zanzibar wana historia ya udugu na ushirikiano. Ukaribu, lugha moja na kuoleana,” alisema Pinda.
Huku akirejea kauli mbalimbali za Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, alisema hata hilo Shirikisho linalopendekezwa litakwama, kwa sababu Rais wake hatakuwa na ardhi, na kama nchi wanachama zitakataa kutoa ardhi, atafanyaje kazi zake.
Alisema tatizo lililopo ni utambulisho wa Zanzibar na suala la umiliki wa ardhi kwa Tanzania Bara wakiwa visiwani, ambayo alisema ni mambo yanayozungumzika.
“Suala hapa ni utambulisho wa Zanzibar ambalo hata hivyo si suala kubwa na tunaweza kulisahihisha. Pia liko suala la ardhi Zanzibar. Lakini wanaotaka ardhi huko, lazima wajiulize je, kweli iko ardhi ya kutosha,” alieleza.
Akizungumzia Bunge Maalumu la Katiba alisema, “Tumeanza mchakato wa kutunga Katiba, lakini tayari kuna changamoto zetu, lakini tumeanza kwa kuchagua Mwenyekiti wa Muda na kutengeneza Kanuni wiki ijayo zitakuwa tayari ili tulifikishe mwisho hili,” alisema na kuongeza:
Bunge Maalumu la Katiba limeanza vikao vyake wiki iliyopita, lakini wiki ijayo linatarajiwa kuanza mijadala baada ya kupitishwa kwa Kanuni na kuchaguliwa kwa Mwenyekiti na hatimaye kuzinduliwa rasmi.
Hata hivyo, tayari kuanza hali ya sintofahamu kwa wabunge kuanzia kudai suala la nyongeza ya posho, hadi katika vikao vyao ya kazi ambako zimeshuhudiwa kauli zinazoashiria kazi nzito mbele na inayopaswa kuwa na udhibiti ili mijadala isitawaliwe na jazba na kutekwa na makundi yaliyowapeleka bungeni humo.
Aliwaomba wajumbe wa semina hiyo ya Jumuiya ya Wazazi kuwaombea wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, watimize majukumu yao kwa maslahi ya Taifa.